MAMA mzazi wa mkongwe wa muziki wa dansi Bongo, Nguza Vicking ‘Babu Seya’ aitwaye Bernadeta, amefariki dunia ghafla mwishoni mwa wiki iliyopita ikiwa ni pigo lingine kwa mwanamuziki huyo na mwanaye, Johnson Nguza ‘Papii Kocha’ wanaotumikia kifungo cha maisha jela.
Kifo hicho kimetokea wakati Babu Seya na Papii Kocha wakiendelea kutumikia kifungo hicho katika Gereza la Ukonga, Dar.
Kwa mujibu wa mtoto wa Babu Seya, Nguza Mbangu, mama huyo alifariki ghafla akiwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) baada ya kusumbuliwa na presha.
Kwa mujibu wa Mbangu, mama wa Babu Seya ambaye ni bibi yake alianza kusumbuliwa na presha baada ya mwanaye na wajukuu zake kutiwa hatiani kwa ubakaji wa wanafunzi wa Shule ya Msingi Mashujaa, Sinza, Dar hadi ugonjwa huo ulipomuondoa ghafla mwishoni mwa wiki iliyopita.
Mbangu alisema kuwa wameumizwa na kifo hicho kwa kuwa marehemu alikuwa tegemeo kubwa kwa ushauri na kifo chake kimezidisha uchungu kwa familia yao.
Mbangu aliongeza kuwa baba yake, Babu Seya na ndugu yake, Papii Kocha waliposikia taarifa hizo walilia kwa uchungu wakiwa gerezani.
Taarifa zaidi zinasema kuwa wanandugu waishio Dar walikutana Kimara, kwa ajili ya kumchagua mwakilishi wa kwenda Kongo kuwahi mazishi.
No comments:
Post a Comment