
Ni wa biashara za silaha zinazoendeshwa barabarani hasa wakati wa foleni huku wengi wao ni vijana wasio na ustaarabu kwa wateja.
Dar es Salaam. Polisi Mkoa wa Kinondoni limeanza msako wa kuwakamata watu wanaofanya biashara ya silaha mbalimbali zinazotumika kwenye uhalifu na kusababisha hofu na vitisho kwa watumiaji barabara.
Akizungumza jana Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni,Charles Kenyela alisema silaha hizo ni pamoja na mapanga,visu na bunduki bandia kuwauzia hasa wenye magari katika makutano ya barabara jambo linalosababisha wengine kutumia mwanya huo kufanya uhalifu. Kamanda Kenyela alisema wamepokea malalamiko kutoka kwa watumiaji wa barabara kufanyiwa uhalifu kwa kuporwa mali mbalimbali wanapokuwa kwenye vyombo vyao vya usafiri. “Tayari tumeshawakamata watuhumiwa wanne katika barabara za Kigogo mwisho na Mburahati kwa kukutwa wakiuza mapanga katika maeneo ya makutano ya barabara hizo,”alisema na kuongeza:
“Msako huu utakuwa endelevu kati ya hao wanaofanya biashara hizo wanatumika katika mitandao ya kihalifu,mfano unaweza ukaonyeshewa biashara ya toi la bastola baadaye wanabadilika na kukuibia na biashara ya mapanga,visu inaweza ikafanyika lakini siyo barabarani iwe sehemu rasmi,”alisema Kenyela.
Alisema kumekuwa na tabia ya baadhi ya vijana kufanya biashara ya kuuza kanda(CD’s au DVD’s) ambazo ni za ngono na zile za uchochezi wa kidini na siasa zinazosababisha mmomonyoko wa maadili na uvunjifu wa amani. “Kwa kuangalia mikanda hiyo ya ngono inasababisha kuongezeka kwa matukio ya ubakaji hasa kwa watoto na kwa upande wa kanda za uchochezi wa kidini na kisiasa zinasababisha uvunjifu wa amani,”alisema Kenyela.
Kamanda Kenyela aliwaomba viongozi wa Serikali za mitaa,madiwani,mgambo,vikundi vya ulinzi shirikishi na wananchi kutoa ushirikiano ili kukomesha biashara hizo zisizofaa katika jamii.
Mwananchi.